Swali Kuu Zaidi Maishani

“Imani katika Kristo ndiyo suluhisho pekee linalofaa dhidi ya hofu ya kifo.”

Kila mwanadamu ana njaa ya kumjua Yule aliyemuumba. Kwa maneno mengine, kila mtu ana hamu ya kumwona Mungu. Kwa mfano – fikiria kinachopita moyoni mwako wakati wowote dhiki au janga linapotokea maishani? Mioyo yetu inatuelekeza kumwita Mtu aliye juu kuliko sisi wenyewe, kutafuta kitu chenye nguvu kuliko sisi wenyewe.

Katika maneno ya mtu mwenye hekima katika Mhubiri 3:11 – Mungu ameweka umilele katika moyo wa mwanadamu.

Kuna maswali mawili makubwa ambayo kila mtu amewahi kujiuliza katika kipindi fulani maishani mwake:
• Maisha ni nini hasa?
• Nini hutokea baada ya maisha kuisha?

Je, unajua jibu la maswali haya? Na ni kwa namna ipi majibu haya – au ukosefu wamajibu haya – kunaathiri maisha yako ya kila siku?

Je, yanapelekea utimilifu na kuridhika katika kazi, mahusiano na familia?

Je, unapata furaha na amani ndani yako – bila kujali hali inayokuzunguka?

Je, una utambuzi wa kusudi unaokupa uhimilifu hata pale unapokabiliwa na majaribu na msiba?

Hebu tuulize swali la kutafakarisha – kama ungeambiwa kwamba leo ni siku yako ya mwisho duniani:
• Ungefanya nini? Ungeenda wapi? Ungesema nini?
• Ingebadilishaje tabia yako, mtazamo wako, mwenendo wako wa maisha?

Ukweli dhahiri ni kwamba siku yoyote – hata leo – inaweza kuwa siku yako ya mwisho duniani. Kifo ni hatima ya kawaida ambayo sote tunaikabili. Je, wazo la kifo linakufanya uogope? Je, una uhakika wa wapi utaishi milele?

Ikiwa moyo wako una njaa juu ya kupata maana katika maisha haya na uhakika wa maisha baada ya kifo, jibu limetolewa na Yesu Kristo!

Kiini cha Ukristo wa kweli ni uhusiano na Yesu Kristo kwa imani – uhusiano unaoendelea hata ng’ambo ya kaburi – kuwaweka huru wale “wale ambao walikuwa utumwani maisha yao yote kwa sababu ya hofu ya kifo.” (Waebrania 2:15).

Lakini Mkristo ni nani hasa? Watu leo hutoa sababu nyingi za kujiita Wakristo.

Kwa mfano, wanasema:
“Mimi ni Mkristo kwa sababu wazazi wangu ni waumini.”
“Mimi ni Mkristo kwa sababu mimi huhudhuria ibada za kanisani wakati wa Pasaka na Krismasi.”
“Mimi ni Mkristo kwa sababu nina uhakika kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu.”
“Mimi ni Mkristo kwa sababu ninajaribu kuwa mtu mwema.”

Tatizo la majibu haya ni kwamba hayataji sababu pekee inayomstahilisha mtu kuwa Mkristo.

Changamoto ni hii hapa:
Unaweza kuhudhuria kanisani na usiwe Mkristo.
Unaweza kusoma Biblia na usiwe Mkristo.
Unaweza kulelewa katika familia ya wacha Mungu na usiwe Mkristo.
Unaweza kuondoa tabia mbaya na kujaribu kuwa mtu mwenye maadili na bado usiwe Mkristo.

Vitendo kama hivyo pekee havimfanyi mtu kuwa Mkristo!

Kuna tofauti kubwa kati ya kujua kuhusu Mungu na kumjua Yeye kikweli.

Mwanadamu ni mwenye dhambi ambaye amepungukiwa na kiwango timilifu cha Mungu. Adhabu ya hili ni kifo – kutenganishwa milele na Mungu. Iwe umejaribu ‘kuwa mtu mwema’ na kudumisha viwango vya Mungu kama ilivyofunuliwa katika Biblia au umeishi maisha bila kujali Mungu au umilele – ukweli ni kwamba sote tumekosa shabaha. Sote tuna deni ambalo hatuwezi kumudu kulipa. Kwa hivyo, sote tunahitaji msamaha Wake sana!

Mungu alikuja duniani katika nafsi ya Yesu Kristo, ambaye aliingia kama mwanadamu na kuishi maisha Yake bila dhambi. Msalabani Kalvari, alikufa kwa ajili yetu na kwa kweli alilipa deni la dhambi zetu! Kupitia imani yetu Kwake, tunapokea:
• Haki Yake,
• Msamaha Wake wa dhambi zetu,
• Zawadi ya uzima wa milele.

Mkristo ni nani basi? Mkristo ni mtu ambaye Mungu amemsamehe kupitia kazi ya Yesu Kristo iliyokamilika Msalabani (Tito 3:3-6).

Hili ndilo jambo kuu:

Kuwa Mkristo si kuhusu unachofanya; ni kuhusu kile ambacho Kristo Yesu amefanya.

Kwa dhabihu Yake isiyo na ubinafsi Msalabani, Yesu alitufanya tufae kwa Mungu na kutustahilisha na Mungu.

Katika Matendo 16:30-31, afisa mmoja wa mamlaka ya kisheria alimuuliza Mtume Paulo swali muhimu zaidi: ‘Nifanye nini ili niokolewe?’ Paulo alijibu kwa unyofu, “Mwamini Bwana Yesu; utaokoka.”

Tunaokolewa na Injili hii ya neema ya ajabu ambayo inasema Yesu anatupenda, alikufa kwa ajili yetu na anatusamehe tunapofungua mioyo yetu kuamini!

Kimbilio lako liko katika maneno haya – Amini Tu!

Unaposoma haya, hali yako ya sasa ikoje?
• Je, unahisi kama maisha yamekulaghai?
• Je, unapambana na masikitiko, kukata tamaa au mfadhaiko?
• Je, unatafuta kusudi kubwa kuliko wewe mwenyewe?

Mtazame Yesu kwa imani! Aliposulubiwa msalabani isivyo haki, Yesu alifanywa kuwa laana uliyostahili (Wagalatia 3:13-14). Alichukua umaskini wako, ugonjwa wako na dhambi yako ili uweze kupokea baraka ambayo Mungu aliahidi kwa wale wanaoshika sheria Yake – ikiwa ni pamoja na utoshelevu mkubwa kwa kila hitaji maishani mwako.

Yesu alimshinda ibilisi pale Kalvari alipofufuka (Wakolosai 2:15)! Ni ushindi wake dhidi ya kifo unaotupa ushindi dhidi ya ibilisi katika maisha yetu ya kila siku hapa duniani na milele Mbinguni!

Unaposikia Neno la Mungu Lililo Hai na kulikumbatia kwa imani, unapokea:
• Uhakikisho wa uhakika wa uzima wa milele pamoja na Kristo,
• Nguvu ya Mungu ya kukabiliana na changamoto za kila siku za maisha,
• Kusudi wazi la kuongoza mipango na maamuzi yako.

Ikiwa moyo wako unasukumwa na ujumbe huu mfupi kumkabidhi Yesu Kristo maisha yako, tunakutia moyo useme sala hii. Iwe uliwahi kuhisi upo karibu na Mungu lakini sasa unahisi uko mbali au hujawahi kujua ukweli wa uhusiano na Yesu Kristo – inatosha kusema sala hii.

Bwana Yesu, nakiri kwamba mimi ni mwenye dhambi. Ninaita jina lako takatifu, Yesu Kristo. Nisamehe dhambi zangu zote. Ninaamini ulikufa badala yangu na ukafufuka kutoka kwa wafu kulingana na Maandiko. Ninakupokea kwa moyo wangu wote. Asante, Bwana kwa wokovu wangu.

Unakaribishwa katika familia ya Mungu! Kumbuka, kumkubali Yesu kama Bwana na Mwokozi wako ni hatua ya kwanza tu katika safari yako ya imani. Kukubali lazima kuambatane na kujitoa! Ni pale tunapojitoa ndipo tunapokuwa wafuasi wa Yesu. Kujitoa ndiko kunasimama kama daraja kati yetu na Yesu.

Ili kukua katika imani, tunakutia moyo kukuza uhusiano wako na Roho Mtakatifu kwa kusoma Biblia yako kila siku. Kadiri unavyosoma kwa saburi, ndivyo utakavyoelewa zaidi kukuhusu wewe mwenyewe na Mungu aliyekuumba! Pia tunakutia moyo kutafuta Kanisa Lililo Hai na kujihusisha nalo.